Sanamu ya Askari au Askari Monument ni sanamu iliyopo penye kitovu cha jiji la Dar es Salaam mahali ambapo mitaa ya Samora na Azikiwe (zamani: Maktaba) zinakutana.
Sanamu inamwonyesha askari Mwafrika katika sare ya kijeshi ya King's African Rifles wakati wa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia (1914-1918) akishika bunduki yenye kisu cha kando na kutazama upande wa bahari.
Sanamu hiyo ni moja kati ya tatu zilizochongwa huko London na mchongaji James Alexander Stevenson kama kumbukumbu ya askari na wapagazi Waafrika waliopiga vita hivyo katika Afrika ya Mashariki hasa kati ya Uingereza na Ujerumani ambao wengi wao walikufa. Zilipelekwa Nairobi, Mombasa na Dar es Salaam[1].
Sanamu ya Dar es Salaam ilisimamishwa kwenye mwaka 1927. Chini yake pana maandishi ya kumbukumbu kwa Kiingereza na Kiswahili kilichoandikwa kwa herufi za Kiarabu na pia kwa herufi za Kilatini. Ni kati ya mifano michache ambako mwandiko wa Kiswahili kwa herufi za Kiarabu unaonekana hadharani.
Maneno yake kwa Kiswahili (kwa herufi za Kiarabu na Kilatini) ni kama yafuatayo:
Sanamu ya Askari ilichukua nafasi ya sanamu ya Wissmann iliyosimamishwa hapohapo mwaka 1909 kwa kumbukumbu ya meja Hermann von Wissmann, gavana wa pili wa Afrika ya Mashariki ya Kijerumani; sanamu hiyo ilibomolewa na Waingereza walipoteka mji katika mwaka 1916.