Makoloni ya Ujerumani mnamo 1914

Ukoloni wa Ujerumani ulijumuisha makoloni ya Dola la Ujerumani nje ya nchi katika kipindi cha kuanzia mwaka 1884 hadi Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia.

Ukoloni wa Kijerumani kabla ya 1871

[hariri | hariri chanzo]

Ujerumani uligawanyika katika madola madogo hadi mwaka 1871 ambako yaliungana chini ya uongozi wa Ufalme wa Prussia kuwa nchi moja.

Jitihada za muda mfupi za ukoloni za nchi kadhaa ndani ya Ujerumani zilifanyika katika karne zilizotangulia, lakini zote ziliachwa hadi kufikia karne ya 18. Brandenburg-Prussia ilijenga boma karibu na Takoradi katika Ghana ya leo kwa biashara ya watumwa lililotumiwa kwa miaka 50 hivi na baadaye kuachwa sawa na vituo vingine.

Jitihada muhimu za ukoloni zilianza tu mwaka 1884 pamoja na juhudi za nchi mbalimbali za Ulaya kugombania Afrika.

Wafanyabiashara na siasa ya nje ya Ujerumani 1871-1880

[hariri | hariri chanzo]

Vyanzo vya ukoloni wa Ujerumani baada ya maungano ya 1871 vilikuwa katika biashara ya kimataifa ya makampuni ya Hamburg na Bremen. Makampuni hayo yalijikuta katika mazingira ambako wafanyabiashara Waingereza na Wafaransa walipata faida kutokana na usaidizi wa serikali zao zilizokuwa na vituo vya kijeshi katika Pasifiki na Afrika ya Magharibi. Tangu miaka ya 1870 wafanyabiashara mbalimbali waliomba serikali ya Dola la Ujerumani wapewe ulinzi. Lakini serikali chini ya chansella Otto von Bismarck ilikataa mara kwa mara kujihusisha na ukoloni.

Pamoja na wafanyabiashara walijitokeza wanasiasa wa mwelekeo wa kizalendo walioona ya kwamba nchi kubwa kama Ujerumani ingestahili kujipatia makoloni kama nchi nyingine za Ulaya. Walikazia uhamiaji wa karne ya 19 ambako Wajerumani milioni 5 waliondoka kwao wakihamia Marekani, Amerika ya Kusini au Australia wakadai makoloni ya Kijerumani kwa shabaha ya kuwatunza wahamiaji kama raia wa Ujerumani. Vyama vya kisiasa vya kizalendo viliingia pia katika bunge la Ujerumani na kutangaza madai hayo pale.

Shirika za kwanza za kiraia za kudai makoloni zilianzishwa zilizojitahidi kuanzia miaka ya 1870. Shirika hizo ziliona mataifa mengine ya Ulaya yalikuwa na makoloni na kupata faida ilhali waliamini Ujerumani ilistahili kuyafuata. Pamoja na hao vyama vya kisiasa vyenye mwelekeo wa kizalendo vilidai pia kupata makoloni. Viliamini ya kwamba Ujerumani ilikuwa na hasara kutokana na uhamiaji wa mamilioni ya Wajerumani waliohamia Marekani, Amerika ya Kusini na Australia na kuwa wananchi wa pale. Iliaminika ya kwamba itawezekana kuwatuma wahamiaji kwenda makoloni ya Ujerumani kama yapo na hivyo kuwatunza kama raia wa taifa.

Tangu mwaka 1880 chansella Bismarck alilegea katika msimamo wake dhidi ya kuhusisha serikali na ukoloni. Mwaka 1882 Uingereza na Ufaransa zilipatana kuhusu maeneo yao katika sehemu za Afrika Magharibi ambako hawakuhusisha wala Waafrika wenyewe wala mataifa mengine yaliyofanya biashara katika sehemu hizo. Hapo wafanyabiashara wa Hamburg na Bremen waliomba serikali tena kutoa ulinzi kwa vituo vya Wajerumani.

Mwaka 1884 Bismarck alikubali maombi ya wafanyabiashara waliofanya mikataba na watawala wadogo wa Kiafrika na kwenye visiwa vya Bahari Pasifiki akawapa barua ya kutambua mikataba yao na kutangaza ulinzi wa serikali yake kwa maeneo husika kwenye pwani za Afrika Kusini-Magharibi (baadaye Namibia), Togo na Kamerun. Katika hatua hii Bismarck hakulenga kuanzisha makoloni aliyoona kuwa na gharama kubwa mno kwa serikali, aliwaza ya kwamba ingetosha kuwasaidia wafanyabiashara wenye mikataba na watawala wa kienyeji na hivyo kuhakikisha faida ya biashara huru kwa makampuni ya Kijerumani. Hii ni sababu ya kwamba Bismark hakukubali jina la "koloni" kwa maeneo alikotoa tangazo la ulinzi, bali aliyaita "Schutzgebiet" (eneo lindwa) lililokuwa jina la makoloni ya Ujerumani hadi mwisho[1].

Upanuzi tangu Mkutano wa Berlin 1885

[hariri | hariri chanzo]

Mwaka 1885 Bismarck aliitisha Mkutano wa Berlin alipolenga kufanya Ujerumani kuwa mpatanishi kati ya nchi za Ulaya zilizoshindana kuhusu Kongo. Wakati wa mkutano alipokea pia ombi la Shirika la Ukoloni wa Kijerumani kukubali madai yao katika maeneo ya Tanganyika; Bismarck alikubali sasa ingawa aliwahi kukataa awali. Kwenye mwisho wa kipindi chake cha kuongoza serikali ya Ujerumani Bismarck alipaswa kutuma wanajeshi waliopigana na wenyeji waliopinga majaribio ya Wajerumani kuchukua utawala juu yao.

Hivyo utawala wa Ujerumani juu ya maeneo katika Afrika, Pasifiki na Asia ulianzishwa ukaendelea haraka kuwa ukoloni kamili ambako Wajerumani walichukua mamlaka yote.

Kwa jumla makoloni ya Ujerumani yalikuwa kama yafuatayo:

Tangu 1919

[hariri | hariri chanzo]

Ujerumani ulipoteza udhibiti wakati wa Vita Kuu ya Kwanza ya Dunia iliyoanza mwaka wa 1914 na makoloni yake yalikamatwa na maadui zake katika vita. Vikosi kadhaa vya kijeshi viliendelea kupigana kwa muda mrefu: Afrika Kusini-Magharibi (leo Namibia) vilisalimisha amri mwaka wa 1915, Kamerun mwaka wa 1916 na jeshi la Schutztruppe la Afrika Mashariki ya Kijerumani tu mwaka wa 1918 mwisho wa vita.

Makoloni ya Ujerumani yalifutwa rasmi katika Mkataba wa Versailles baada ya kushindwa kwa Ujerumani katika vita. Maeneo yote yalikabidhiwa kama maeneo ya kudhaminiwa chini ya usimamizi wa Shirikisho la Mataifa kwa nchi washindi yaani Uingereza, Ufaransa, Ubelgiji, Afrika Kusini, Australia, Japani na Marekani.

Marejeo

[hariri | hariri chanzo]
  1. Rudin, Germans in the Cameroons, uk 39

Kujisomea

[hariri | hariri chanzo]
Makala hii kuhusu mambo ya kihistoria bado ni mbegu.
Je, unajua kitu kuhusu Ukoloni wa Ujerumani kama enzi zake au matokeo yake?
Labda unaona habari katika Wikipedia ya Kiingereza au lugha nyingine zinazofaa kutafsiriwa?
Basi unaweza kuisaidia Wikipedia kwa kuihariri na kuongeza habari.