Lugha (kutoka neno la Kiarabu: لغة) ni utaratibu wa kuwasiliana kati ya binadamu (wengine wanadai hata kati ya viumbe wenye akili).
Somo la lugha linaitwa maarifa ya lugha au isimu.
Mwaka wa 2008 ulikuwa Mwaka wa Lugha wa Kimataifa.
Lugha ni mfumo wa sauti za nasibu zenye maana na zilizokubaliwa na jamii ya watu fulani ili zitumike katika kuleta mawasiliano.
Lugha ni mfumo wa sauti za nasibu kwa sababu zilitokea kama bahati tu kwa binadamu. Wanyama hawatumii lugha kama chombo cha mawasiliano, kwa kuwa lugha ni sauti zenye maana na kukubaliwa na jamii.
Hakuna lugha bora zaidi duniani, kwa kuwa lugha zote zina ubora, mradi zikidhi matakwa ya jamii husika.
Mbali na maana ya kawaida kuna pia lugha ya ishara inayotumiwa na watu bubu. Katika fani ya programu za kompyuta ni kawaida kuongea juu ya " lugha ya kompyuta".
Lugha huwa na tabia zifuatazo:
Kimsingi lugha ni moja. Uwasilishwaji wake ndio huigawa katika tanzu/aina kuu mbili:
Hii ni lugha ambayo huwasilishwa na watu kwa njia ya mazungumzo ya mdomo - na hurithishwa kutoka kizazi kimoja hadi kingine kwa njia ya mazungumzo. Lugha ya mazungumzo ni kongwe, hai na halisi zaidi ya mzungumzaji na ina maana nyingi, kwani mzungumzaji na msikilizaji huwa ana kwa ana katika mazingira mamoja.
Stadi za lugha ya mazungumzo ni kuzungumza na kusikiliza.
Na. | Chanzo | Kikomo |
---|---|---|
1 | Kuzungumza | Kusikiliza |
2 | Mzungumzaji | Msikilizaji |
Hii ni lugha ambayo huwasilishwa kwa njia ya maandishi. Hii ni kiwakilishi cha lugha ya mazungumzo katika mfumo wa maandishi. Lugha ya maandishi ni changa kwani imeanza milenia za hivi karibuni baada ya kuvumbuliwa kwa maandishi.
Stadi za lugha ya maandishi ni kuandika na kusoma:
Na. | Chanzo | Kikomo |
---|---|---|
1 | Kuandika/Maandishi | Kusoma |
2 | Mwandishi | Msomaji |
Kwa kawaida, lugha ni sehemu ya utamaduni wa umma fulani. Lugha ya aina hii inaitwa lugha asilia. Lakini pia kuna lugha za kuundwa.
Lugha ina nyanja kuu mbili, nazo ni:
Tangu siku za kwanza za binadamu, lugha zimekuwa zikichipuka, kukua, kutangaa na kufa kama kiumbe yeyote mwingine. Kwa hivyo, lugha zilizopo leo ulimwenguni, huenda baada ya karne nyingi kupita zikatoweka na kuzuka nyinginezo.
Leo ulimwenguni mathalan, kuna lugha karibu 6,700, zikiwa 1,000 katika bara la kaskazini na la kusini la Amerika, 2,000 zikiwa kwenye bara la Afrika, 230 katika bara la Ulaya, 2,200 katika bara la Asia, na 1,300 katika bara la Oshania (Australia na nchi jirani nayo).