Milki ya Wasasani au Nasaba ya Wasasani (Kiing. Sassanids au Sassanians) ni jina linalotumika kwa nasaba ya Uajemi ya Kale (leo Iran) ambayo ilidumu kutoka 224 hadi 651 BK. [1] [2]
Milki ya Wasasani ilifuata Waparthi kama watawala wa Uajemi. Ilitambuliwa kwa zaidi ya miaka 400 kama moja ya falme mbili kubwa huko Asia Magharibi, pamoja na Dola la Roma na baadaye Ufalme wa Byzanti.
Mfalme wa kwanza wa Kisasani alikuwa Ardashir I aliyewahi kuwa mtawala wa kieneo katika jimbo la Pars kwenye nyanda za juu za kusini ya Uajemi; eneo ambako kumbukumbu ya watawala wa Liakhemi kabla ya uvamizi wa Wagiriki miaka 500 iliyopita ilikuwa hai bado. Ardashir alimpindua mfalme wa Waparthi aliyewatazama kama wageni kutoka kaskazini akalenga kurudisha ukubwa wa Uajemi wa Kale chini ya Waakhemi[3].
Wasasani waliendelea kutumia jiji la Ktesiphon katika Mesopotamia (Iraki ya leo) kama mji mkuu[4].
Wasasani walifufua Uzoroasta kama dini rasmi ya milki yao, na kwa vipindi kadhaa walitesa Wakristo walioanza kuenea katika milki yao. Walipigana vita vingi dhidi ya Dola la Roma na baada ya mgawanyiko wa Roma, dhidi ya Ufalme wa Bizanti. Wakati huohuo walipaswa kupigana na mashambulio ya makabila kutoka Asia ya Kati.
Vita hizi nyingi zilichosha nguvu ya milki, na baada ya vita ya miaka 30 dhidi ya Roma, Wasasani walikosa nguvu kujitetea dhidi ya uvamizi wa Waislamu kutoka jangwa la Uarabuni.
Walijenga utamaduni mkubwa ulioshawishi pia majirani yake na hata Waarabu waliovamia na kutawala maeneo yao kama sehemu ya ukhalifa wao.
Nasaba ya Wasasani ilianzishwa na Ardashir I wakati alikuwa amemshinda mfalme wa mwisho wa Waparthi, Artabanus IV. Ilikwisha wakati shahanshah (mfalme mkuu) wa mwisho wa Kisasani, Yazdegerd III (632-651), alishindwa baada ya vita ya miaka 14 dhidi ya uvamizi wa Waarabu Waislamu.
Maeneo ya Milki ya Wasasani yalijumuisha Iran ya leo, Iraki, Armenia, Afghanistan, sehemu za mashariki mwa Uturuki, na sehemu za Syria, Pakistan, Kaukazi, Asia ya Kati na Bara Arabu.
Enzi ya Wasasani inachukuliwa kuwa moja ya vipindi muhimu na vyenye ushawishi katika historia ya Iran. Kwa njia nyingi kipindi cha Wasasani kilipata mafanikio ya hali ya juu zaidi ya ustaarabu wa Kiajemi. Ikaunda Dola kuu la mwisho la Kiajemi kabla ya uvamizi wa Kiarabu na uenezaji wa Uislamu.
Uajemi uliathiri sana ustaarabu wa Kiroma wakati wa enzi za Wasasani, [5] p109 na Waroma waliwawekea Waajemi Wasasani pekee hadhi ya usawa. Kaisari wa Roma alimwandikia Shah wa Uajemi barua ambamo alimtaja kama "ndugu yangu".
Ushawishi wa Wasasani ulienea hadi kufika Ulaya Magharibi, Afrika, [6] China na Uhindi, pamoja na kuathiri sanaa ya zamani ya Ulaya na Asia. [7]
Ushawishi huo uliendelea katika utamaduni wa karne za kwanza za Uislamu. Mengi ya yale ambayo baadaye yalijulikana kama utamaduni wa Kiislamu pamoja na usanifu, uandishi na ustadi mwingine ulikopwa haswa kutoka kwa Waajemi Wasasani na kuenezwa katika maeneo mengine ya Waislamu.
226-241: Utawala wa Ardashir I:
241-271: Utawala wa Shapur I:
271-301: Kipindi cha mapambano ya kinasaba.
283: Vita na Roma. Waroma wanachoma Ktesiphon.
296-298: Vita dhidi ya Roma. Uajemi inaachia Roma majimbo matano mashariki mwa mto Hidekeli
309-379: Utawala wa Shapur II "Mkuu":
387: Armenia iligawanyika katika maeneo ya Kiroma na ya Kiajemi.
399–420: Utawala wa Yazdegerd I "mtenda dhambi":
420-438: Utawala wa Bahram V:
438-457: Utawala wa Yazdegerd II:
482-3: Uasi wa Kiarmenia na Iberia ya Kaukazi
483: Wakristo wanapewa uvumilivu
484: Peroz I anashindwa na kuuawa na Waheftali.
491: Uasi wa Kiarmenia. Kanisa la Kitume la Armenia linakataa Mtaguso wa Kalsedonia:
502-506: Vita dhidi ya Bizanti.
526-532: Vita dhidi ya Bizanti.
531-579: Utawala wa Khosrau I, "mwenye roho isiyokufa" (Anushirvan)
540-562: Vita dhidi ya Bizanti.
572-591: Vita dhidi ya Bizanti. Uajemi hutoa sehemu kubwa ya Armenia na Iberia kwa Bizanti.
590-628: Utawala wa Khosrau II
603-628: Vita kuu dhidi ya Byzanti. Uajemi inachukua Mesopotamia, Syria, Palestina, Misri na maeneo ya Kaukazi, kabla ya kurudishwa nyuma na Wabizanti hadi mipaka ya kabla ya vita.
610: Waarabu wanashinda jeshi la Wasaani huko Dhu-Qar.
626: Kuzingirwa kwa Bizanti - Konstantinopoli na Waajemi wakisaidiwa na Waavari.
627: Kaisari wa Bizanti Heraklio anavamia Mesopotamia. Kushindwa kwa uamuzi wa vikosi vya Uajemi kwenye mapigano ya Ninawi.
628-632: Kipindi cha machafuko cha watawala wengi.
632-642: Utawala wa Yazdegerd III.
636: Kushindwa kwa Wasasni katika mapigano ya al-Qadisiyyah wakati wa uvamizi wa Waislamu katika Uajemi.
642: Ushindi wa mwisho wa Waarabu juu ya jeshi la Uajemi huko Nahavand (Nehavand).
651: Mtawala wa mwisho wa Kisasani, Yazdegerd III anauawa huko Merv, Turkmenistan ya leo. Mwisho wa nasaba. Mwanawe Piruz na wengine wengi wanakimbilia uhamishoni nchini China.
((cite web))
: CS1 maint: date auto-translated (link)